MST-Department of Kiswahili and African Languages

Permanent URI for this collection

Browse

Recent Submissions

Now showing 1 - 20 of 293
  • Item
    Mchango wa Mashairi ya Kiswahili katika Ukuzaji. wa Stadi ya Kuongea katika Shule za Upili, Kaunti ya Murang’a, Kenya
    (Kenyatta University, 2017-09) Macharia, Charles Gitonga; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Kiswahili poems are a major component of the Kiswahili syllabus in secondary schools in Kenya. Kiswahili poems are taught as a section of literature from Form One to Form Four. The purpose of this research was to investigate the role of Kiswahili poems in the teaching and learning of Kiswahili speaking skills in Kangema Sub County, Murang'a County. The specific objectives were to establish the role of Kiswahili poems in the teaching and learning of speaking skills, to investigate the methods used by teachers to teach Kiswahili poems in enhancing the learners speaking skills, to establish the learners and teachers perceptions towards Kiswahili poems, to investigate the effects of those perceptions in the teaching and learning of Kiswahili speaking skills and to identify any challenges faced by teachers in the teaching of Kiswahili poems. The study used the dialogism theory advanced by Mikhail Mikhailovich, (1895- 1975). This theory is used to explain the relationship between pronunciation and the meaning of different statements. The study used a descriptive survey design. The target population was 25 schools, 1300 form 3 students, 77 teachers of Kiswahili, 25 principals and one Education Officer. The sample size was 30% of the total population, that is 8 schools, 390 students, 24 teachers, 9 principals and I Education Officer. Random sampling was used to select the students, stratified sampling to select schools and purposive sampling to select the education officer. Research instruments included student’s questionnaires, teachers and principals questionnaires, an observation checklist for the avalability of teaching and learning resources and an interview guide for the education officer. Data analysis was done according to the objectives of the research using the Scientific Package for Social Sciences method (SPSS). Positive responses were separated from negative responses using percentages. The results were presented using percentages, graphs, charts, tables and discussion. The findings of this research are that Kiswahili poems play a significant role in developing the speaking skills of learners. Learners should be involved more in reciting and chanting Kiswahili poems so that they can get used to the correct pronunciation.The research recommends that learners should be encouraged to participate in music festivals so that they can recite and chant Kiswahili poems, The Ministry of Education should add more lessons to Kiswahili so that time can be created for Kiswahili poems. This research is aimed at providing an alternative way to the teachers’, students, curriculum developers and other stakeholders in the education sector on how speaking skills can be learned and taught effectively using Kiswahili poetry.
  • Item
    Taharuki na Sadfa katika Ujenzi wa Maudhui katika Riwaya za Mwana B’a Yungi Hulewa na Tutarudi na Roho Zetu
    (Kenyatta University, 2022-06) Maroko, Christopher Orina; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Utafiti huu ulishughulikia matumizi ya taharuki na sadfa katika ujenzi wa maudhui katika riwaya za Mwana wa Yungi Hulewa (1976) na Tutarudi na Roho Zetu (1987) zilizoandikwa na Muhammed Said Abdulla na Ben Mtobwa mtawalia. Utafiti huu ulikusudia kuchunguza namna taharuki na sadfa zimetumika kujenga maudhui ya riwaya teule. Malengo ya utafiti yalikuwa kubainisha aina za taharuki zilizotumika katika riwaya teule, kuchanganua aina za sadfa zilizotumika katika riwaya teule na maudhui yaliyojengwa katika riwaya za Mwana wa Mwana wa Yungi Hulewa (1976) na Tularudi na Roho Zetu (1987). Utafiti huu uliongozwa na nadharia ya uhakiki wa kimtindo kwa mujibu wa Leech (1969). Nadharia ya uhakiki wa kimtindo huchunguza namna mtindo hutumiwa na mtunzi katika kujenga maudhui. Katika utafiti huu, mbinu kusudio iliturnika kuteua aina za taharuki na aina za sadfa zilizotumiwa katika riwaya teule. Aidha, maudhui yaliyojengwa katika riwaya teule yaliangaziwa. Data iliyochanganuliwa ilipatikana kwa kusoma riwaya teule. Data hii ilichanganuliwa kwa kuzingatia mihimili ya nadharia ya uhakiki wa kimtindo kwa kuainisha na kuchanganuaaina za taharuki na aina za sadfa zilizotumika na matokeo kuwasilishwa kwa njia ya maelezo. Uchunguzi huu ulibainisha kuwa: taharuki na sadfa ni muhimu katika kujenga maudhui ya riwaya za kipelelezi, taharuki hutanguliza maudhui yanayoandikiwa na huibua masuala halisi katika jamiina sadfa hupelekea riwaya za kipelelezi kiafikia kilele chake. Utafiti huu ni muhimu kwa kuwa utasgidia wanaosoma kuelewa kuwa taharuki na sadfa huweza kuainishwa kwa mujibu wa wataalamu mbalimbali. Aidha uchunguzi buu utasaidia kufahamu namna taharuki na sadfa zimetumika kujenga maudhui katika riwaya za kipelelezi
  • Item
    Usawiri wa Mhusika Mkinzani katika Tamthilia Teule za Ebrahim Hussein: Kinjeketile (1969), Jogoo Kijijini (1976) na Arusi (1980)
    (Kenyatta University, 2024-11) Oluchili, Wilson; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Utafiti huu umechunguza usawiri wa mhusika mkinzani katika tamthilia teule za Ebrahim Hussein; Kinjeketile (1969), Jogoo Kijijini (1976) na Arusi (1980). Mhusika mkinzani ni mhusika ambaye huenda kinyume cha maadili ya jamii yake au kukinzana na mhusika nguli katika kazi ya fasihi. Katika kufanya hili, mkinzani hukuza kutoelewana au mgogoro katika utungo wa kifasihi. Malengo yaliyonuiwa kutekelezwa ni; kubainisha mbinu mbalimbali za usawiri wa mhusika mkinzani katika tamthilia teule, kuchunguza namna mhusika mkinzani anavyokuza mgogoro katika tamthilia teule na kutathmini maudhui yanayoibuliwa na mhusika mkinzani katika tamthilia teule. Nadharia mbili ndizo zilizoongoza utafiti huu; Naratolojia na nadharia ya Drama. Naratolojia iliasisiwa na Plato (1930) na kukuzwa na Rimmon-Kennan (1983), Stanzel (1984), Phelan (1987) na Keen (2003). Inahusika na vipengele vya usimulizi vikiwemo wakati, nafsi, nafasi, wahusika na maudhui. Vipengele vya wahusika na namna wanavyokuza maudhui ndivyo vilivyotufaa katika utekelezaji wa lengo la kwanza na la tatu. Naratolojia inafafanua kuhusu njia za kuwasawiri wahusika na vilevile kueleza kuhusu wahusika kama vyombo vya kuwasilishia ujumbe (maudhui). Hata hivyo, swala la ukuzaji wa mgogoro na mhusika mkinzani halielezeki vyema na nadharia ya Naratolojia. Hivyo, nadharia ya Drama iliyoasisiwa na Carl Jung (1964) ndiyo iliyotuongoza katika kutekeleza lengo la pili. Nadharia hii ya Drama inahusu matendo ya wahusika katika drama na namna yanavyopelekea kuzuka kwa migogoro. Sampuli iliteuliwa kwa mbinu ya kimaksudi ambapo tamthilia mbili; Kinjeketile na Jogoo Kijijini ziliteuliwa kimaksudi ili kuchunguza usawiri wa mhusika mkinzani kama mhusika asiyekuwepo kwenye jukwaa. Kwa upande mwingine, tamthilia ya Arusi iliteuliwa ili kuchunguza usawiri wa mhusika mkinzani kama mhusika aliyepo kwenye jukwaa. Data ilikusanywa maktabani ambapo tasnifu, majarida na makala mbalimbali yanayohusiana na mada hii yalisomwa kwa kina. Aidha data ya kimsingi ilitoka katika tamthilia teule ambazo zilisomwa na kuchanganuliwa kwa umakini na uzingativu mwingi. Hoja zinazohusiana na mkinzani zilitengwa katika mada ndogondogo, zikachanganuliwa kisha kufafanuliwa kwa maelezo yaliyoambatanishwa na dondoo mwafaka kutoka katika tamthilia teule. Jumla ya ripoti ya utafiti huu imesukwa katika sura tano. Matokeo ya kazi hii yanatarajiwa kuwafahamisha wasomi kuhusu mbinu mbalimbali za kumsawiri mhusika mkinzani katika tamthilia pamoja na nafasi yake katika ukuzaji wa mgogoro na maudhui. Utafiti uligundua kwamba, mhusika mkinzani katika tamthilia anaweza kuwasilishwa kama mhusika aliyepo kwenye jukwaa au kama mhusika asiyekuwepo kwenye jukwaa. Mhusika mkinzani anapowasilishwa kama mhusika asiyekuwepo kwenye jukwaa, huzua ukinzani kutokana na wanachokisema wahusika wengine au msimulizi kuhusu matendo yake. Haya yalibainishwa katika tamthilia za Kinjeketile na Jogoo Kijijini. Aidha, iligundulika kuwa mhusika mkinzani anapowasilishwa kama mhusika aliyepo kwenye jukwaa, huzua ukinzani kutokana na mazungumzo na matendo yake ya moja kwa moja kama ilivyobainika katika Arusi. Mbinu ambazo mhusika mkinzani amesawiriwa nazo katika tamthilia teule ni pamoja na ya kuwatumia wahusika wengine, ya kinatiki, ya kimaelezo na ya ulinganuzi na usambamba. Pia, mkinzani amebainika kuwa nguzo muhimu katika ploti ya tamthilia kwani huchochea migogoro mikuu katika drama. Mbali na hayo, utafiti umeonyesha kwamba, katika tamthilia teule, mhusika mkinzani ametumiwa na mtunzi kama chombo cha kuwasilishia maudhui makuu, kama vile udhalimu, ukatili, usaliti, siasa na utawala kwa ujumla.
  • Item
    Tathmini ya Maigizo ya Wahusika Walemavu Katika Kipindi cha Sultana Kwenye Runinga ya Citizen Nchini Kenya
    (Kenyatta University, 2025-09) Getate, Caroline Kemunto; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Kipindi cha Sultana kilipeperushwa kwenye runinga ya Citizen nchini Kenya kuanzia Machi, 2022 hadi Julai, 2023. Kipindi hicho kilihusisha wahusika mbalimbali wakiwemo walemavu. Tafiti za awali zimechunguza usawiri wa wahusika walemavu katika njia hasi. Utafiti huu ulilenga kuziba pengo hilo kwa kuchunguza usawiri wa wahusika walemavu kwenye vipindi vya televisheni kwa njia chanya. Hivyo basi, utafiti huu ulilenga kuchunguza maigizo ya wahusika walemavu kwenye kipindi hicho. Suala la utafiti lilikuwa kutathmini maigizo ya wahusika walemavu katika kipindi cha Sultana katika runinga ya Citizen nchini Kenya. Malengo ya utafiti huu yalikuwa; kujadili maudhui yanayowasilishwa na wahusika walemavu katika kipindi cha Sultana kwenye runinga ya Citizen, pili, kubainisha sifa za wahusika walemavu katika kipindi cha Sultana kwenye runinga ya Citizen na kufafanua mbinu za maigizo zinazotumika na wahusika walemavu katika kipindi cha Sultana kwenye runinga ya Citizen. Utafiti huu uliongozwa na nadharia ya Maigizo (Turner, 1969) inayosisitiza umuhimu wa kudhihirisha mitagusano ya wanajamii kwenye maisha yao halisi kupitia matendo yao kwenye jukwaa. Aidha, nadharia hii inaonyesha manufaa ya hadhira katika kuchunguza vitendo vya waigizaji kwenye jukwaa. Utafiti huu ulifanywa maktabani na nyanjani. Maktabani mtafiti alidurusu vitabu, majarida, tasnifu na miswada mbalimbali kuhusu uigizaji, mbinu za utafiti na nadharia ya Maigizo. Utafiti wa nyanjani ulihusu ukusanyaji wa data kwa kuhusisha mahojiano na kurekodi. Vifaa vya utafiti vilivyotumiwa ni simu ya rununu, tarakilishi na mwongozo wa mahojiano. Jumuiya ya utafiti ilikua waigizaji walemavu wa viungo na wa tabia wa kipindi cha Sultana cha runinga ya Citizen. Sampuli ya utafiti iliteuliwa kimaksudi ili mtafiti aweze kupata data ya malengo ya utafiti. Data ilikusanywa kwa kutazama, kusikiliza na kunukuu majibu ya maswali kutoka kipindi kiteule. Data ilichanganuliwa kwa njia ya maelezo kwa kuzingatia nadharia ya Maigizo, maswali na malengo ya utafiti. Matokeo ya utafiti yaliwasilishwa kimaelezo. Utafiti ulibaini kuwa wahusika walemavu wa viungo na wa tabia wanawasilisha maudhui mbalimbali. Wahusika walemavu wanawasilisha maudhui ya bidii, mapenzi, ujasiri na unyanyapaa ilhali wale wa tabia wanawasilisha maudhui ya ukatili, mauaji, tamaa na utabaka. Utafiti pia umeonyesha kuwa wahusika walemavu wana sifa mbalimbali wanazotumia kuwasilisha maudhui. Wahusika walemavu wa viungo wanadhihirisha kuwa na ukakamavu, hasira, ubinafsi, upweke, uvumilivu na hekima ilhali wale wa tabia wanadhihirisha kuwa na taasubi ya kiume, ukatili, udanganyifu, tamaa, ukaidi na uchochezi. Aidha, mbinu mbalimbali zilitumiwa na wahusika walemavu. Mbinu hizi ni pamoja na kufananisha, ishara za mwili, mazungumzo na hisia na mielekeo ya wahusika. Utafiti huu utasaidia kuongeza data muhimu katika taaluma ya fasihi. Pia, utawafaa watafiti watakaotumia nadharia ya Maigizo kwa kurejelea mihimili yake ambayo mtafiti amejadili kwa kina.
  • Item
    Usawiri wa Wahusika Vimada Katika Riwaya Teule za John Habwe: Mfano Kutoka kwa Paradiso (2005), Cheche za Moto (2008) na Safari ya Lamu (2011)
    (Kenyatta University, 2025-06) Munguti, Catherine Ndinda; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Utafiti huu umechunguza usawiri wa vimada katika riwaya teule za John Habwe. Riwaya zilizoteuliwa katika utafiti huu ni zifuatazo: Paradiso (2005), Cheche za Moto (2008) na Safari ya Lamu (2011). Riwaya hizi ziliteuliwa kutokana na motifu ya wahusika vimada wanaobainika wakiwemo Sakina, Fatuma na Maimuna mtawalia. Uchunguzi wa usawiri wa vimada ulikuwa muhimu kwa sababu ni suala ibuka katika jamii ya kisasa. John Habwe ameziandika riwaya zenye kuwaibua wahusika vimada wanaoishi na wanaume nje ya misingi ya ndoa. Tafiti mbalimbali zimefanywa kuhusu usawiri wa wahusika katika utanzu wa riwaya ya Kiswahili. Baadhi ya tafiti hizi ni pamoja na Muindi (1990), Saro (2017), Mavisi (2019) na Kanwa (2022). Tafiti hizi zimeeleza usawiri wa wahusika wa wanawake kwa jumla katika riwaya. Hata hivyo, hazijaweza kufafanua usawiri wa wahusika vimada jambo ambalo limefanywa na utafiti huu. Malengo ya utafiti huu ni: kufafanua usawiri wa wahusika vimada katika riwaya teule, kubaini vichocheo kwa wahusika kuwa vimada na kuchanganua athari za hali ya maisha ya wahusika vimada katika riwaya teule. Utafiti huu uliongozwa na nadharia ya uhalisia. Nadharia ya Uhalisia iliasisiwa na Georg Lukacs (1938). Nadharia hii hueleza ukweli kama ulivyo katika jamii. Mihimili ya nadharia ya uhalisia iliufaa utafiti huu kwa kuonyesha kuwa John Habwe anawachora wahusika vimada kama wanavyojitokeza katika jamii. Data ya kimsingi ilitoka kwenye riwaya teule. Riwaya teule zilisomwa ili kupata kauli na matendo ya wahusika vimada. Utafiti huu ni wa kimaelezo ambapo kila lengo lilichanganuliwa katika sura yake mahususi kwa kuihusisha mihimili ya nadharia ya Uhalisia. Utafiti huu ulifanyiwa maktabani ambapo vitabu, tasnifu na majarida yalisomwa pamoja na kusakura mitandao ili kupata tafiti zilizokuwa za punde zaidi kote ulimwenguni. Utafiti umegundua kuwa wahusika vimada wamesawiriwa kwa hali chanya katika mahusiano yao na wahusika wengine katika riwaya teule. Isitoshe, utafiti umebaini kuwa wahusika vimada katika riwaya teule wameathiri maisha ya wahusika wengine kwa namna chanya na kuishia kuboresha hali ya maisha ya wahusika wanaokaa nao kinyumba. Utafiti huu unatarajiwa kutoa mchango katika uhakiki wa utanzu wa riwaya kuhusu usawiri wa wahusika katika riwaya ya Kiswahili.
  • Item
    Wakaa, Uwasilishaji Usemi na Wahusika katika Hotuba Teule za Wanasiasa wa Kenya
    (Kenyatta University, 2025-11) Mukonambi, Kekonen Stanley; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Utafiti huu ulichunguza wakaa, uwasilishaji usemi na wahusika katika hotuba teule za wanasiasa wa Kenya. Baadhi ya wanasiasa hutumia hotuba zinazovuta makini ya wasikilizaji na wafuasi wao kwa mitindo tofauti. Mojawapo ya mbinu hizi za kimtindo ni usimulizi. Utafiti huu ulichunguza vipengele vya usimulizi; wakaa, uwasilishaji wa usemi na wahusika. Wakaa ni mpangilio wa matukio katika hadithi. Uwasilishaji wa usemi ni namna ambavyo maana hutolewa kwa kutumia lugha ilhali wahusika ni viumbe wa kisanaa wanaoendeleza kazi ya kifasihi. Malengo ya utafiti huu ni: kubainisha vipengee vya wakaa, uwasilishaji wa usemi na wahusika katika hotuba teule na kujadili dhima ya wakaa, uwasilishaji usemi na wahusika katika hotuba teule. Nadharia iliyotumika ni ya Naratolojia kwa kuzingatia mawazo yake Rimmon-Kenan. Mtazamo wake ni wazi kwani huwasaidia wasomaji kutofautisha kwa urahisi viwango vya masimulizi na kuchanganua matini kwa hatua. Aidha, haujatumika na tafiti nyingi ikilinganishwa na ule wa Gerald Genette. Mihimili yake ilifaa kwani iliweka wazi vipengele ambavyo vilishughulikiwa na kutathmini nafasi yavyo katika uelewekaji wa hotuba teule. Uteuzi wa sampuli kimaksudi ulitumika kuteua hotuba teule za Rais mstaafu Uhuru Kenyatta wa chama cha TNA na JP, Mhes. Raila Odinga wa chama cha ODM na Rais Dkt. William Ruto wa chama cha URP, JP na UDA zilizotolewa kati ya mwaka 2013 hadi 2023. Utafiti ulifanyika maktabani ambako data ilikusanywa kwa njia za usomaji makini kwa kupitia makala, nyaraka, majarida, tasnifu za awali na kutazama na kusikiza makala ya mtandao wa YouTube. Ufafanuzi wa kimaelezo kwa kuzingatia nadharia ulitumiwa kutolea matokeo ya utafiti ambayo yamewasilishwa kwenye vijimada vilivyomo katika sura tano za tasnifu hii. Matokeo ya utafiti huu yanatoa mchango katika taaluma ya fasihi kwa wahakiki na wanafunzi kufahamu nafasi ya vipengee hivi katika hotuba. Aidha, unawafaidi wahakiki na watafiti wa fasihi kwa kuwaelekeza jinsi ya kuhakiki hotuba.
  • Item
    Tathmini ya Sura za Ufisadi Katika Riwaya za Tom Olali Mafamba (2012) na Watu wa Gehenna (2012)
    (Kenyatta University, 2025-11) Musyoki, Pauline Kamanthe; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Utafiti huu unafafanua sura tofauti za ufisadi. Mtafiti amefanya hivi kwa kushughulikia riwaya ya Mafamba (Olali, 2012) na Watu Wa Gehenna (Olali, 2012). Ufisadi ni suala tata ulimwenguni na hata nchini Kenya. Dhana hii ni pana ila maelezo yake katika fasihi ni finyu kwa kuwa, msisitizo umekuwa kwenye matumizi ya fedha za umma.Kulingana na Tume ya EACC (2016) kipengele cha iv, ufisadi unahusu unyanyasaji katika ofisi za umma, upendeleo, hongo, ulaghai, ukosefu wa uaminifu katika ofisi za umma, kutolipa ushuru au ada yoyote ile na kutofuata sheria zilizohidhinishwa kuteua viongozi katika ofisi za umma. Mtafiti ameangazia masuala hayo kwa kutathmini riwaya teule kwa lengo la kubainisha namna masuala hayo yalivyosawiriwa na kuleta uwezekano wa sura tofauti za ufisadi. Wahakiki kama vile; Muthumbi (2005), Ochenja (2008), Mayieka (2015), Sereti (2016), Mwaniki (2018) na wengineo wameeleza ufisadi kama matumizi mabaya ya fedha za umma na ndio sababu utafiti huu umeangazia sura tofauti za ufisadi. Riwaya zimeteuliwa kimakusudi na zimeangazia sura tofauti za ufisadi hivyo zilitupa data mwafaka. Nadharia ya Uhalisia wa Kijamaa na Udenguzi zilitumika. Nadharia ya Uhalisia wa Kijamaa inahusishwa na Karl Marx na fikra zake zilitokana na zile za mwanafalsafa Hegel (1971). Waitifaki wake ni Gorky, Baxandall, Terry, James Bisztray na wengine.Kumekuwa na ufisadi katika jamii yoyote ya kitabaka tangu Ujima,Utumwa ,Umwinyi, Ubepari, Ujamaa na Ukumiunisti. Nadharia hii hivyo basi ilitumika kuangazia mfumo wa kiuchumi ambapo kuna tabaka la juu na chini. Tabaka la juu huwa na mifumo ya uzalishaji mali. Njia wanazotumia kumiliki mali ni ufisadi. Tabaka la juu hukiuka maadili ya kiutawala wakijinufaisha na kudhalilisha watu wa tabaka la chini. Kwa kuwa nadharia hii inaelezea uhalisia kama ulivyo, haikuwezesha kutafuta maana zinginezo za ufisadi hivyo nadharia ya Udenguzi ilimfaa mtafiti kuangazia fasiri mbalimbali za ufisadi. Nadharia ya Udenguzi iliasisiwa na Jacques Derrida (1962).Waitifaki wake ni pamoja na Foucault, Roland Barthes, Jean Baudrillard Paul de Man, J.Hillis Miller, Jacques Lacan, Barbara Johnstone na wengineo. Kupitia mihimili ya nadharia hii mtafiti alieleza fasiri mbalimbali za ufisadi. Utafiti huu ulifanywa maktabani kwa kusoma vitabu teule, tasnifu, majarida na makala ya mitandaoni yanayohusiana na mada. Data ya kimsingi ilitolewa kwenye riwaya teule. Data hiyo ilichanganuliwa kwa kuzingatia malengo na nadharia zinazoongoza utafiti. Matokeo yamewasilishwa kwa kutumia njia ya maelezo. Utafiti huu utakuwa muhimu kwa wasomi na jamii kwa jumla hasa kwa kuagazia suala tata la ufisadi
  • Item
    Tathmini ya Uainishaji wa Tanzu na Vijitanzu vya Fasihi Simulizi katika Vitabu Vilivyoidhinishwa: Kaunti ya Makueni
    (Kenyatta University, 2025-10) Munyao, Carolyne Nzilani
    Utafiti huu unahusu tathmini ya uainishaji wa tanzu na vijitanzu vya fasihi simulizi katika vitabu vilivyoteuliwa kufunza fasihi simulizi ya Kiswahili kwa walimu na wanafunzi katika Shule za Upili Kenya, Kaunti ya Makueni. Utafiti ulilenga kuonyesha ukinzano wa idadi ya tanzu na vijitanzu na matatizo yanayokumba wanafunzi na walimu katika uainishaji wa fasihi simulizi. Masuala matatu yalilengwa katika utafiti huu: kubainisha tofauti katika uainishaji wa tanzu na vijitanzu vya fasihi simulizi katika vitabu vilivyoidhinishwa, kubainisha vigezo vilivyotumiwa na kupendekeza suluhisho kwa utata unaotokana na tofauti hizi za uainishaji. Nadharia mbili zilitumiwa:ya Tanzu na ya Ujifunzaji na Upokeaji wa Lugha ya Pili (Second Language Learning and Acquisition) iliyoasisiwa na Krashen (1982) ambapo haipothesia ya mchakato (Input hypothesis) zilitumiwa kufanikisha malengo ya utafiti huu. Haipothesia hii ilihusu sheria katika upokezi wa lugha, kusonga kutoka kwa dhana rahisi hadi ngumu na uelewa wa maarifa kutoka (i+1) ambapo i ni maarifa yaliyopo tayari na 1 ni maarifa yanayopatikana baadaye kupitia ujifunzaji. Nadharia ya Tanzu ilijikita kwa maswali je, tanzu zipo? Je, kuna idadi mahsusi ya tanzu? na Je, tanzu zinajisimamia au zinaingiliana? Nadharia hii ililenga uainishaji wa tanzu na vigezo vya uainishaji. Uteuzi wa kimakusudi ulitumiwa kuteua vitabu vilivyoidhinishwa na taasisi ya kukuza mitaala vya kufundishia fasihi simulizi kwa shule za upili, vitabu hivi viliwapa watafiti data ya kimsingi (maktabani) ilhali data endelezi (nyanjani) ilitokana na wanafunzi na walimu. Shule nne za upili ziliteuliwa ambapo wanafunzi ishirini wa kidato cha nne walihojiwa. Aidha, walimu wawili wa Kiswahili katika kila shule waliteuliwa na kuhojiwa. Muundo wa utafiti huu ni wa kimaelezo. Data iliyopatikana ilichanganuliwa kwa mtindo wa kimaelezo na kuwasilishwa kwa maelezo fafanuzi na majedwali. Matokeo ya utafiti huu yalibainisha kuwa vitabu tofauti vilivyoidhinishwa kufundishia fasihi simulizi kwa shule za upili vilikuwa na uainishaji unaotofautiana wa tanzu na vijitanzu vya fasihi simulizi. Baadhi ya vitabu vina tanzu nne, vingine tano na vingine sita. Pamoja na hayo, utafiti ulibaini kuwa uainishaji wa tanzu na vijitanzu vya fasihi simulizi unategemea vigezo na misingi mbalimbali inayofuatwa na wataalamu katika kuandika matini za fasihi simulizi kama vile; muundo, maudhui, wakati, mtindo, wahusika na kadhalika. Ilibainika kuwa, ni kwa sababu hii kunatokea utata katika vitabu vilivyoidhinishwa. Kwa mujibu wa nadharia ya Ujifunzaji na Upokeaji wa Lugha ya Pili, iwapo mada zitawasilishwa kwenye vifaa kwa njia isiyo wazi basi kutakuwa na changamoto kwa wasomaji. Aidha, kupitia hojaji, wasailiwa walikiri kuwa kuna utata katika ufundishaji na usomaji wa fasihi simulizi kutokana na hali hii. Hivyo basi, mtafiti alipendekeza kuwa, mada za fasihi simulizi zinastahili kuratibiwa upya ili ziwafae wanafunzi na walimu katika shule za upili. Utafiti huu ni wa manufaa kwa watafiti, wahakiki, waandishi wa vitabu vya fasihi simulizi, walimu na wanafunzi wa Shule za Upili na waratibu wa mitaala.
  • Item
    Mielekeo ya Wauza Mifugo Mnadani Wanaozungumza Kinandi Kuhusu Kiswahilikatika Kaunti ya Nandi
    (Kenyatta University, 2025-11) Jepkemboi ,Anne; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Utafiti huu ulilenga kueleza jinsi mielekeo ya wauza mifugo mnadani katika kaunti ya Nandi kuhusu lugha ya Kiswahili inavyoathiri matumizi yao ya lugha. Mwelekeo wa watu kuhusu vitu au dhana unaweza kuathiri wale watu au dhana hizo. Tafiti tofauti zilizofanywa kuhusu mielekeo ya watu kwa lugha zimebaini kuwa mielekeo ya watu huweza kuwa hasi au chanya kutegemea masiala mbalimbali kama vile elimu, umri, mazingira, jinsia na kadhalika. Utafiti huu uliongozwa na malengo yafuatayo: kupambanua mielekeo ya wauza mifugo mnadani wanaozungumza Kinandi kwa lugha ya Kiswahili katika kaunti ya Nandi; kubainisha mambo ambayo husababisha mielekeo ya wauza mifugo mnadani wanaozungumza Kinandi kuhusu lugha ya Kiswahili na kuchunguza athari ya mielekeo hiyo ya lugha kwa maendeleo ya Kiswahili katika jamii hii. Nadharia ya Utendaji Razini (Theory of Reasoned Action) iliyoasisiwa na Fishbein na Ajzen (1975) ilitumiwa kuongoza utafiti huu. Wataalamu hawa wanasema kuwa binadamu ni viumbe wanaofikiria na wanajua aina ya mielekeo na tabia walizo nazo. Kwa hivyo, maelezo ya watafiti hawa yanalingana na lengo la utafiti huu ambalo ni kueleza matumizi ya Kiswahili miongoni mwa wauza mifugo mnadani ambao mielekeo yao hudhihirika kupitia matumizi yao ya lugha. Utafiti huu ulihusisha wauza mifugo 35 kutoka minada yote 7 katika kaunti ya Nandi. Mtafiti alitumia idadi hii kimaksudi. Utafiti huu ulitumia mbinu ya utafiti wa maelezo ambapo data ilikusanywa kupitia hojaji, mahojiano na kushiriki utendaji kisha ikachanganuliwa na kuwasilishwa kupitia majedwali, baa grafu na pai chati. Ilibainika kwamba wauza mifugo mnadani wana mitazamo hasi kuhusu utumiaji wa Kiswahili kwa sababu wanahisi Kiswahili ni kigumu kwao. Matokeo ya utafiti huu yanaweza kutumiwa na washikadau mbalimbali wanaohusika na lugha ili kuweka mikakati ya kuhakikisha kuwa Wakenya wote wanafahamu na kutumia kwa ufasaha lugha ya Kiswahili ili wabadili mielekeo yao hasi kuhusu lugha hii.
  • Item
    Maudhui ya Ukungwi katika Nyimbo Teule za Taarab
    (Kenyatta University, 2025-11) Wendo, Fadhili Hamisi
    Utafiti huu umechunguza jinsi maudhui ya ukungwi yanavyojitokeza katika nyimbo teule za taarab. Malengo yafuatayo yalinuiwa kutekelezwa; kubainisha dhima ya kungwi katika jamii ya Waswahili, kuchunguza maudhui ya ukungwi katika nyimbo teule za taarab na kulinganisha dhima ya kungwi na maudhui ya ukungwi katika nyimbo teule za taarab. Sampuli iliteuliwa kimaksudi ambapo kati ya nyimbo nyingi za taarab, nne ndizo ziliteuliwa kutumika katika utafiti huu. Nyimbo hizi ni: Maji ya Uvuguvugu (Wachonga Vinyago), Nenda salama (Omar Kopa), Ndoa (Aslay na Khadija Kopa), Bi Harusi (AT). Sampuli ya utafiti huu iliteuliwa kwa kutumia mbinu ya kimakusudi. Kati ya maeneo mengi katika jamii ya Waswahili, eneo la Msambweni ndilo lililoteuliwa kutumika katika utafiti. Mbinu hii ilifaa katika kuwateua makungwi waliochangia data muhimu ya kuchanganuliwa. Utafiti huu uliongozwa na nadharia mbili; nadharia ya Simiotiki na nadharia ya Uamilifu. Nadharia ya Simiotiki iliasisiwa na Ferdinand Dessaussure (1913) na Charles Pierce (1977) na inahusu uhusiano uliopo kati ya kitaja na kitajwa na matumizi ya ishara, picha na msimbo. Nadharia hii ilisaidia katika kufafanua mbinu za uwasilishaji wa ujumbe katika nyimbo teule za taarab. Kwa upande mwingine nadharia ya Uamilifu iliasisiwa na Emile Dukheim (1912) na inahusika na uchambuzi wa dhima zinazojitokeza katika kazi za fasihi. Hii ilituongoza katika kubainisha dhima ya kungwi katika jamii. Utafiti huu ulikuwa wa kimaktaba na wa nyanjani ambapo maktabani; mtafiti aliweza kusoma tasnifu, makala na majarida yanayohusiana na mada. Nyanjani, mtafiti alitembelea eneo lengwa ili kuwahoji baadhi ya makungwi kuhusu dhima yao. Matokeo yalionyesha kuwa kungwi ana jukumu la kuwafundisha wanawali kuhusu maswala ya unyumba yakiwemo usafi wa mwili na nyumba, namna ya kumhudumia mume, namna ya kusema na marafiki na jamaa za mume, matumizi ya vifaa vya kiasili kama vile mbuzi, kinu, mchi ufagio miongoni mwa mengine. Aidha, maudhui haya ya ukungwi yanafundishwa na waimbaji wa nyimbo teule za taarab na kuonyesha namna kipera cha nyimbo na mawaidha vinaingiliana kimaudhui. Utafiti huu unatarajiwa kutoa mchango wa kuonyesha jinsi vitanzu vya mawaidha na nyimbo huingiliana kidhima.
  • Item
    Mtazamo Linganishi WA Itikadi Katika Utenzi WA Mwanakupona na Mashairi Ya Muyaka
    (Kenyatta University, 2025-11) Mutembei, Doreen Nkatha
    Utafiti huu ulilenga kulinganisha itikadi katika mashairi ya Muyaka na Utenzi wa Mwanakupona. Dhana ya itikadi ni dhana changamano na pana na imeibua mijadala mingi baina ya wataalamu mbalimbali. Itikadi ni muhimu kwa sababu huelekeza matendo yote ya mtunzi kuhusu yale atakayowasilisha na namna atakavyowasilisha kazi yake. Kwa hivyo, itikadi ndio huongoza misimamo, mielekeo na imani ya mtunzi. Vitabu teule vya kufanikisha utafiti huu ni mashairi ya Muyaka na Utenzi wa Mwanakupona. Vitabu hivi viliteuliwa kwani ingawa kazi hizi ziliandikwa katika kipindi kimoja, ni tofauti kimtindo na kimaudhui. Hivi ni kusema kuwa watunzi hawa waliongozwa na itikadi tofauti. Kwa hivyo, ni muhimu kuchunguza na kuzilinganisha zile itikadi katika mashairi ya Muyaka na Utenzi wa Mwanakupona na jinsi itikadi husika zinazowaongoza watunzi hao zinavyolingana na kujitokeza katika kazi zao. Utafiti huu uliongozwa na malengo yafuatayo: kubaini itikadi katika Utenzi wa Mwanakupona na mashairi ya Muyaka, kutathmini jinsi athari za itikadi zinavyopelekea uwasilishaji wa maudhui kwenye Utenzi wa Mwanakupona na mashairi ya Muyaka na kuchunguza athari za itikadi katika uwasilishaji wa mtindo katika mashairi ya Muyaka na Utenzi wa Mwanakupona. Nadharia ya itikadi, mikabala ya Karl Marx (1977 na 1979), Louis Althusser (1981) na Antonio Gramsci (1985) ilitumika. Mkabala wa Karl Marx umetumika kwani unashikilia kuwa itikadi ni ‘ungamuzi potoshi.’ Mkabala wake Louis Althusser umetumika kwani aliorodhesha vyombo vya kiitikadi ambavyo alivigawa katika vikundi viwili. Vinavyo endeleza itikadi moja kwa moja kama vile polisi, jeshi, mahakama na serikali. Pia, vyombo visivyo vya moja kwa moja kama dini, elimu, vyombo vya habari na familia. Mwisho, mkabala wake Antonio Gramsci umetumika kwani Gramsci anaieleza dhana hii ya itikadi kama fikra, mitazamo na mielekeo ambayo binadamu huchukulia kuwa za kawaida hivyo kujikandamiza kwa hiari yake mwenyewe. Data husika ilitolewa maktabani ambapo shairi, beti, mishororo na vipande vya mishororo vilivyo na dhana za kiitikadi zilikusanywa. Mbinu ya usampulishaji wa kimaksudi ilitumika katika uteuzi wa sampuli. Data ilichanganuliwa na kuwasilishwa kwa njia ya kimaelezo ili iweze kueleweka. Kutokana na data ya utafiti huu, imebainika kuwa Muyaka na Mwanakupona waliongozwa na itikadi tofauti ingawa walikuwa watunzi wa kipindi kimoja cha kirasimi. Itikadi hizo zilipelekea uwasilishaji wao wa maudhui na mtindo vitofauti.
  • Item
    Majazi na Stiari katika Riwaya ya Dunia Yao na Nyuso za Mwanamke
    (Kenyatta University, 2024-12) Mathuku, Joseph
    Utafiti huu ulichunguza matumizi ya majazi na stiari katika riwaya mbili teule za Said Ahmed Mohamed nazo ni Dunia Yao (2006) na Nyuso za Mwanamke (2010). Utafiti huu ulilenga kubaini majazi na stiari katika kazi teule, nafasi ya majazi na stiari katika kuwasawiri wahusika na kuonyesha jinsi mtunzi ametumia tamathali hizi kuibua maudhui. Utafiti huu ulikuwa wa kimaelezo na wa maktabani. Uteuzi wa sampuli ulikuwa wa kimakusudi ukilenga riwaya za Said Ahmed Mohamed nazo ni Dunia Yao (2006) na Nyuso za Mwanamke (2010). Ukusanyaji wa data ulihusisha usomaji wa kina wa riwaya teule ili kupata data inayokusudiwa. Hizi ni riwaya ambazo zimesheheni matumizi ya majazi na stiari. Data ilichanganuliwa kwa kuongozwa na malengo ya utafiti pamoja na mihimili ya nadharia ya Mtindo na ile ya Matumizi ya Stiari. Nadharia ya Mtindo inashikilia kuwa kazi za kifasihi haziwezi kuibuliwa bila matumizi ya lugha nayo nadharia ya Matumizi ya Stiari hushikilia kuwa ili kuelewa dhana moja ya kistiari yafaa tuilinganishe na nyingine iliyo na sifa zile zile zinazorejelewa. Uwasilishaji wa data hiyo ulikuwa wa kimaelezo. Riwaya ya Dunia Yao (2006) na ile ya Nyuso za Mwanamke (2010) tulizozitafitia ziliandikwa mwanzo mwanzo wa Karne ya 21 na zilidhihirisha mkondo mpya wa kutunga kazi za kifasihi (ule wa usasa baadaye). Riwaya hizi zilisheheni matumizi mapya na ya kipekee ya majazi na stiari ambapo uwasilishaji wa uhalisia na usawiri wa wahusika sasa haufanywi kwa kufuata mkondo wa hurafa kama hapo awali bali unahusisha matumizi mapya ya majazi na stiari ambapo hadithi, wahusika, matukio na mandhari huweza kufasiriwa au kusomwa ili ziweze kuleta zaidi ya kiwango kimoja cha maana. Utafiti huu utawafaa wahakiki wa riwaya ya Kiswahili, wasomi na watunzi wa kazi za kifasihi kuona namna waandishi wa tungo za kifasihi wa Karne hii ya 21 wanavyotumia tamathali za usemi kwa njia ya kipekee kuwasilisha uhalisia.
  • Item
    Uchanganuzi Linganishi wa Matini ya Hotuba za Kisiasa Kuhusu Ufisadi Kuanzia Mwaka 2015 Hadi 2020
    (Kenyatta University, 2025-06) Mworeh, Felix Shimenga; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Hotuba ni chombo muhimu kinachotumiwa na wanasiasa kuwasilisha sera zao, itikadi na hata kukemea maovu yanayotendeka katika jamii. Nchini Kenya, suala la ufisadi ni mojawapo ya maovu yanayotekelezwa na baadhi ya viongozi na wananchi. Kwa sababu hii, wanasiasa wengi huliangazia suala hili katika hotuba zao kwa umma kama mojawapo ya mikakati ya kuupiga vita ufisadi. Wao hutumia lugha kwa njia ya kipekee wanapoangazia suala hili hususan vita dhidi yake. Hii basi ndiyo sababu utafiti huu ulilenga kuchanganua na kulinganisha matini ya hotuba za kisiasa zinazoangazia suala la ufisadi nchini Kenya. Utafiti uliongozwa na nadharia ya Uchanganuzi Usemi Hakiki (UUH) iliyoasisiwa na Fairclough katika kuchanganua hotuba sita za viongozi wawili wa kisiasa wa nchi ya Kenya kuhusu ufisadi ili kuchanganua na kulinganisha namna matini ya hotuba za kisiasa yanavyoshughulikia suala la ufisadi, kubainisha athari za hotuba hizi kwa wananchi na kisha kubaini mielekeo ya wananchi kuhusu hotuba hizi. Usampulishaji wa kimakusudi ulitumiwa kuwachagua wasailiwa na pia viongozi wa kisiasa ambao matini za hotuba zao zilichanganuliwa na kulinganishwa. Wanasiasa teule ni wale ambao wameliangazia suala hili la ufisadi kwa kina, hivyo basi hotuba zao ni faafu katika utafiti huu. Ili kupata matini za hotuba za kisiasa ambazo zilitumiwa kama data katika utafiti huu, mtafiti alikusanya video kutoka mtandao wa “YouTube”. Data nyingine pia ilikusanywa nyanjani kupitia hojaji funge ya likati na hojaji wazi ili kubaini athari na mielekeo ya wananchi wa Kenya kuhusu hotuba za kisiasa zinazoangazia suala la ufisadi. Mtafiti alizisikiliza na kuzinukuu hotuba teule kisha kuchanganua na kulinganisha matini zake. Aidha, data ilichanganuliwa na kulinganishwa kwa kutumia majedwali, takwimu na maelezo na kisha matokeo yake kuwasilishwa vilevile kwa kutumia maelezo, majedwali na takwimu. Matokeo ya utafiti huu yatawapa wananchi ama matumaini kuwa hotuba za kisiasa zinatekeleza dhima kuu katika vita dhidi ya ufisadi au ni gumzo tupu. Utafiti huu pia utachangia katika taaluma ya uchanganuzi matini ya hotuba za kisiasa zinazolenga maudhui teule kwa kutumia nadharia ya Uchanganuzi Usemi Hakiki.
  • Item
    Kanuni za Lugha Zinavyoathiri Somo la Kiswahili Katika Shule za Upili: Mfano za Kaunti ya Busia
    (Kenyatta University, 2025-04) Osodo, Elizabeth Auma; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Utafiti huu ulishughulikia mielekeo ya wanafunzi na walimu wa shule za upili katika Kaunti ya Busia kuhusu kanuni za lugha shuleni na namna kanuni hizi zinavyoathiri somo la Kiswahili. Utafiti huu ulichunguza na kuhakiki kanuni za lugha katika shule za upili. Aidha ulibaini mielekeo ya wanafunzi na walimu kuhusu kanuni za lugha shuleni na athari yake kwa somo la Kiswahili. Malengo matatu yalioongoza utafiti huu ni: Kueleza kanuni za lugha shuleni, kuchunguza mielekeo ya wanafunzi na walimu kuhusu kanuni za lugha shuleni na kufafanua athari za kanuni za lugha shuleni kwa somo la Kiswahili katika shule zilizo Kaunti ya Busia.Utafiti huu ulitumia nadharia mbili katika uchanganuzi wa data. Kwanza, nadharia ya Saikolojia ya jamii ya Vitendo Vilivyofikiriwa ya Ajzen na Fishbein (1980). Nadharia hii inasema kuwa, binadamu huwa na mtazamo kubalifu kuhusu jambo ambalo litamnufaisha na kuwa na mwelekeo hasi kwa jambo ambalo halina manufaa kwake. Nadharia hii ilitumika kubainisha mielekeo ya walimu na wanafunzi kuhusu kanuni za lugha za shule. Nadharia hii haingeweza kuhakiki kanuni za lugha za shule na athari yake kwa somo la Kiswahili kwa kukosa vigezo vya kuchanganua data hii. Kwa hivyo, nadharia ya pili ambayo ni ya Kijumuia na Kibinadamu ilioasisiwa na Richards na Rodgers (1995) ilitumika. Nadharia hii inasema kuwa, mazingira yenye usalama na utu kwa mwanafunzi humwathiri anapojifunza lugha ya pili. Ili kufanikisha malengo ya utafiti, wanafunzi na walimu kutoka shule za upili saba zenye viwango vya Kitaifa, Zaidi ya Kaunti na Kaunti ziliteuliwa. Walimu na wanafunzi walijaza hojaji likati na wanafunzi kushiriki katika mjadala elekezi wa makundi. Utafiti huu ulihusisha wanafunzi 560 na walimu saba wa somo la Kiswahili ambao pia ni wakuu wa idara ya Kiswahili. Mtafiti pia alifanya mahojiano na walimu wakuu kwa kila shule kuhusu kanuni za lugha zilizoteuliwa. Utafiti uliteua shule tatu za wasichana za bweni, tatu za wavulana za bweni na shule moja ya mseto ya kutwa. Utafiti huu ulifanywa nyanjani na maktabani. Vifaa tofauti vilitumiwa nyanjani, hojaji likati ilitumika ili kubainisha mielekeo ya walimu na wanafunzi kuhusu kanuni za lugha za shule. Mjadala elekezi wa makundi ulitumika kubainisha sababu ya mielekeo chanya au hasi na manufaa ya kanuni za lugha za shule kwa wanafunzi. Mbinu ya uchunzaji ilitumika kwa kutazama mabango yaliyo shuleni na kuchunguza namna mijadala kwa lugha ya Kiswahili ilivyoendeshwa. Utafiti wa maktabani ulifanywa kwa kusoma kazi za waandishi mbalimbali zinazohusu sera ya lugha kwa jumla, kanuni za lugha shuleni pamoja na mielekeo yao. Uchanganuzi wa data ulifanywa kwa kuainisha mada tofauti tofauti. Njia ya maelezo ilitumika kuwasilisha data kwa kiasi kikubwa. Picha, majedwali na michoro pia ilitumika. Matokeo ya utafiti yalionyesha kuwa, shule tofauti zina kanuni za lugha tofauti na utekelezaji wake pia ni tofauti. Kanuni hizi ni kama lugha ya mawasiliano katika mazingira ya shule, siku za Kiswahili, mabango na maandishi katika mazingira ya shule, matumizi ya lugha ya Kiswahili katika mijadala, shughuli za idara ya Kiswahili kama makongamano, usomaji wa vitabu na magazeti pamoja na vyama vya Kiswahili. Ilibainika kuwa, wanafunzi na walimu wana mielekeo chanya kwa kanuni za lugha za shule ambazo zinaimarisha matokeo ya mtihani katika somo la Kiswahili. Utafiti pia ulibaini kuwa, utekelezaji wa kanuni za lugha za shule unahitaji mchango na ushirikiano wa wizara ya elimu, uongozi wa shule, walimu na wanafunzi wote ili athari yake iwe chanya kwa somo la Kiswahili.
  • Item
    Itikadi Kama Chanzo cha Migogoro katika Msimu Wa Vipepeo K.W Wamitila (2006) na Mhanga Nafsi Yangu S.A Mohamed (2013).
    (Kenyatta University, 2025-04) Moses, Grace Mwende; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Utafiti huu ulishughulikia itikadi kama chanzo cha migogoro katika riwaya ya Msimu wa Vipepeo (2006) yake K.W Wamitila na Mhanga Nafsi Yangu (2013) yake S.A Mohamed. Utafiti huu ulinuia kuonyesha itikadi kama chanzo cha migogoro miongoni mwa wahusika katika riwaya teule. Tafiti tofauti zimefanywa na wataalamu kuhusiana na suala la migogoro katika riwaya ya Kiswahili. Hata hivyo, kadri ya ufahamu wa mtafiti haupo utafiti ambao umeangazia itikadi kama chanzo cha migogoro. Aidha, riwaya teule hazijachambuliwa kwa kuangazia mtazamo huu. Utafiti huu ulinuia kuchanganua itikadi kama chanzo cha migogoro katika riwaya teule, kutathmini athari za migogoro hii katika uwasilishaji wa maudhui na ploti katika riwaya na kujadili suluhu za migogoro hiyo kwa kuangazia riwaya teule. Utafiti huu uliongozwa na nadharia ya Hejemonia iliyoasisiwa na mwanafalsafa Antonio Gramsci (1985). Mihimili ya nadharia hii ilikuwa ni, Hejemonia hutegemea makubaliano yaliyopo kati ya watawala na wanaotawaliwa, asasi za kijamii hutumiwa na tabaka tawala kuwapumbaza raia na Hejemonia huendelezwa kupitia kwa tamaduni za jamii husika. Mihimili hii ilimwezesha mtafiti kuichanganua data kwa ukamilifu. Mbinu ya kimaelezo ndiyo iliyotumiwa katika uchanganuzi wa data. Matokeo ya utafiti huu yameafikiana na yaliyotarajiwa katika utafiti huu kwa kudhibitisha kuwa itikadi ndizo chanzo cha baadhi ya migogoro iliyopo katika riwaya teule. Ni wazi kuwa, migogoro ambayo chanzo chake ni itikadi huibua maudhui tofauti na humsaidia mwandishi kuijenga ploti katika kazi yake. Mwisho, baadhi ya migogoro katika riwaya inaweza kusuluhishwa kwa kutumia mbinu tofauti ambazo ziliangaziwa. Matokeo ya utafiti huu yatakuwa ya manufaa kwa wasomi, watafiti na waandishi wa riwaya ya kiswahili kwa kukuza maarifa yao kuhusu suala la migogoro na itikadi za wahusika katika riwaya.
  • Item
    Maudhui katika Nyimbo Zilizopendwa za Kiswahili: Mtazamo Linganishi wa Daudi Kabaka Na Kikundi cha Maroon Commandos
    (Kenyatta University, 2025-02) Malelu, Onesmus Kioko
    The research intended to investigate themes in popular Swahili songs: A comperative approach of Daudi Kabaka and Maroon Commndos group. The songs were sang between the year 1960 and 1990. The research was guided by realism theory. The researcher went through recorded songs stored in round discs. Selected literary materials were also read for the purposes of getting data. The collected data was recorded and analysed guided by the research questions and objectives. The report was presented in five chapters. Chapter one includes the study topic, research questions, objectives of the study, justifications for the study, scope of the study, literature review and theoretical framework. The second chapter analyses themes in Daudi Kabaka and Maroon Commandos group songs. Chapter three examines how language use has aided in making the themes come out clearly. The fourth chapter examines the comparisons found between the works of the two artists. The fifth chapter includes summery, conclusion and recommendations for further research. This research will benefit other literary scholars and current artists to make their work better.
  • Item
    Upokezi wa Taswira za Matangazo ya Biashara katika Runinga: Kata Ndogo za Nyali na Likoni Kaunti ya Mombasa, Kenya
    (Kenyatta University, 2025-06) Omuhonja, Elizabeth Nipher; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Utafiti huu ulichunguza upokezi wa taswira za matangazo ya biashara katika runinga. Matangazo kumi ya biashara yanayotangazwa kwa lugha ya Kiswahili yalichunguzwa pamoja na yale ambayo yanachanganya Kiswahili na lugha nyingine. Malengo ya utafiti huu yalikuwa ni kubainisha taswira zinazotumika kwenye matangazo yanayohusu bidhaa za nyumbani katika runinga, kuchanganua taswira zinazotumika kwenye matangazo yanayohusu huduma za mawasiliano katika runinga na kutathmini fasiri za watazamaji kuhusu taswira mbalimbali zilizoteuliwa kwa kuzingatia umri, jinsia na elimu. Sababu ya kufanya utafiti huu ni kuwa swala la kuonyesha namna mbinu ya taswira inavyotumika katika matangazo ya biashara kwa madhumuni ya kuathiri upokezi wa bidhaa zinazotangazwa halijachunguzwa kwa kina. Kazi hii iliongozwa na nadharia mbili; nadharia ya semiotiki iliyoasisiwa na Barthes (1984) inayohusu uhakiki wa ishara na nadharia ya ya upokezi iliyoasisiwa na Iser (1974) inayosisitiza nguvu za mpokeaji au msomaji katika kufasiri kazi anayoipokea na hutilia maanani dhima yake kwa kazi hiyo. Uchunguzi ulifanyika maktabani na nyanjani. Maktabani usomaji wa vitabu, tasnifu, makala na majarida yanayohusu mada ulifanyika kwa kina. Nyanjani data kuhusu fasiri mbalimbali za taswira ilikusanywa kwa kutumia hojaji katika maeneo ya Nyali na Likoni ili kuzitathmini. Matokeo ya utafiti yametolewa kwa njia ya kimaelezo na majedwali. Matokeo ya utafiti yalionyesha kuwa watangazaji wa matangazo ya biashara hutumia taswira kwa wingi katika matangazo hayo ili kupitisha ujumbe kwa hadhira. Taswira zinazotumika haswa za ishara huhitaji umakinifu wa hali ya juu kutoka kwa hadhira ili waweze kuzifasiri vyema. Taswira za ishara zilipata fasiri mbalimbali kutoka kwa hadhira kwa kuzingatia vigezo vya, umri, jinsia na kiwango cha elimu. Matokeo ya utafiti huu yamewasilishwa katika sura tano. Utafiti huu umetoa mchango kwa wasomi na watafiti kwa kuonyesha namna mbinu ya taswira inavyotumika katika matangazo ya biashara kwa lengo la kuathiri upokezi wake.
  • Item
    Uchanganuzi wa Kiisimu katika Mashairi Huru ya Kithaka wa Mberia na ya Kezilahabia
    (Kenyatta University, 2025-06) Wafula, Pouline Nangila; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Lengo kuu la utafiti huu ni kuonyesha jinsi ushairi unavyoweza kuchanganuliwa kiisimu. Tasnifu hii inahusu uhakiki wa kiisimu wa ushairi wa Kiswahili katika mashairi huru ya Kithaka wa Mberia na ya Kezilahabi kwa mtazamo wa nadharia ya Fonolojia Mizani. Utafiti huu umejikita katika diwani teule za watunzi waliotajwa ambazo ni Doa, Msimu wa Tisa, Mvumo wa Helikopta, Kichomi na Karibu Ndani. Uteuzi wa diwani hizi ulifanywa kimakusudi kwa kuwa zina aina data iliyodhamiriwa kuchanganuliwa kiisimu ambayo ilitosheleza mahitaji ya utafiti huu. Mashairi sitini yalihakikiwa kutoka katika diwani teule. Vipengele vya kiisimu vilivyochanganuliwa ni: Aina za sentensi, kipengele cha nafsi na uakifishaji. Utafiti huu uliongozwa na nadharia ya Fonolojia Mizani iliyoasisiwa na Liberman (1975) ambayo ina madai kuwa mkazo katika lugha uko katika mfumo wa mfuatano wiani wa kimsonge ambao hupanga silabi, maneno na virai katika sentensi. Tasnifu hii ina sura nne: Sura ya kwanza imeangazia utangulizi unaojumulisha vipengele vifuatavyo: mada, suala la utafiti, maswala ya utafiti, malengo ya utafiti, umuhimu wa utafiti, sababu za kuchagua mada, upeo na mipaka ya utafiti, yaliyoandikwa kuhusu mada, misingi ya nadharia, mihimili ya nadharia na mbinu za utafiti. Sura ya pili imeshughulikia vipengele vya kiismu vilivyobainishwa na jinsi vinavyotumika katika kuendeleza kazi ya mashairi huru teule ya Kithaka wa Mberia. Sura ya tatu imebainisha vipengele vya kiisimu na kuonyesha jinsi vilivyotumika katika kuendeleza mashairi huru ya Kezilahabi. Sura ya nne imeshughulikia umuhimu wa vipengele vya kiisimu kisha sura ya tano imeshughulikia muhtasari wa utafiti, matokeo ya utafiti, changamoto za utafiti na mapendekezo ya taifi zaidi. Data iliyotumika katika utafiti huu ilikusanywa kutoka maktabani. Maktabani ndiko usomaji ulifanywaa wa diwani za mashairi teule, tasnifu na vitabu vingine vinavyohusiana na mada ya utafiti na nadharia ya utafiti huu. Uchanganuzi wa data ulifanywa kwa kutumia mbinu ya uhakiki matini kwa kuongozwa na pengo la utafiti, maswali na malengo ya utafiti na kwa kuongozwa na mihimili ya nadharia ya Fonolojia Mizani. Kwa kufanya hivi, utafiti uligundua kwamba mbinu za kiisimu zinaweza kutumiwa katika uhakiki wa mashairi huru ya Kiswahili.
  • Item
    Usawiri wa Mandhari Katika Diwani ya Doa
    (Kenyatta University, 2025-06) Gitonga, Doris Gakii; King'ei, Kitula Osore, Miriam
    Utafiti huu ulishughulikia usawiri wa mandhari katika katika Diwani ya Doa na jinsi mandhari hayo yamechangia katika uwasilishaji wa ujumbe wa mwandishi. Utafiti huu ulilenga kubainisha jinsi mtunzi alivyotumia aina tofauti za mandhari katika kukamilisha ujumbe wake. Utafiti huu umebainisha wazi mandhari mbalimbali katika diwani ya Doa (2018). Aidha, utafiti hu umedhihihirisha namna mandhari hayo yalivyosawiriwa kwa kuweka wazi umuhimu wake katika kukamilisha ujumbe wa mtunzi. Utafiti huu ulichunguza aina za mandhari katika diwani ya Doa (2018). Nadharia ya Naratolojia ndiyo iliyoongoza utafiti huu. Naratolojia iliyoasisiwa na Genette (1972) na baadaye kuendelezwa na De Jong (2012). Nadharia ya Naratolojia huchunguza sifa za muundo wa usimulizi kwa kugawa vipengele ambavyo huhusiana na simulizi kisha kuzingatia uhusiano na uamilifu baina ya vipengele hivyo. Data iliyotumiwa katika uchunguzi huu ilitoka maktabani na mtandaoni. Kwa maktaba, mtafiti alisoma yale yanayohusiana na mada lengwa yakiwemo tasnifu, majarida na vitabu vinginevyo hasa vinavyo husiana na nadharia husika. Mtandaoni mtafiti alisoma baadhi ya tafiti zinazohusiana na mada teule na yanayohusu utanzu wa ushairi. Sampuli kusudio ni nakala ya diwani ya Doa (2018) ambayo ilikuwa muhimu sana katika utafiti huu. Yaliyotokea katika utafiti huu yametolewa kwa maelezo ya kinathari na utoaji wa mifano. Matokeo ya utafiti huu yamepangwa katika sura tano. Matokeo ya utafiti huu yanatarajiwa kuchangia pakubwa katika fasihi ya Kiswahili hasa utanzu wa ushairi kwa kuonyesha aina za mandhari na nafasi yake katika ukuzaji wa maudhui.
  • Item
    Athari ya Tamthilia ya Mashetani (1971) juu ya Tamthilia ya Mashetani Wamerudi (2016)
    (Kenyatta University, 2025-05) Nyanchama, Filister Eunice
    Utafiti huu ulilenga kuchunguza athari ya tamthilia ya Mashetani (1971) juu ya tamthilia ya Mashetani Wamerudi (2016). Kristeva (1966) anafafanua kuwa hakuna matini yoyote ya kifasihi inaweza kuangaliwa kivyake au kujitegemea. Hivyo basi, ilikuwepo haja kuangazia athari ya dhamira, maudhui, wahusika na mtindo katika tamthilia hizi teule. Utafiti huu uliongozwa na nadharia ya Mwingilianomatini ilioasisiwa na Kristeva (1966). Mwingilianomatini ni kutegemeana na kuathiriana kwa tanzu au matini (Kuloba, 2015). Hivyo basi, mwingilianomatini ni wakati ambapo sifa za matini moja huweza kujitokeza katika matini nyingine. Mtafiti aliongozwa na malengo yafuatayo: Kwanza, kubainisha athari ya kimaudhui katika tamthilia ya Mashetani na tamthilia ya Mashetani Wamerudi. Pili, kuchunguza athari ya usawiri wa kiwahusika katika tamthilia ya Mashetani na Mashetani Wamerudi. Tatu, kuchanganua athari ya kimtindo katika tamthilia ya Mashetani na tamthilia ya Mashetani Wamerudi. Mbinu ya utafiti iliyotumika ni ya kimaelezo ambapo mtafiti alibainisha matukio au data mbalimbali katika tamthilia ya Mashetani na Mashetani Wamerudi. Data iliyokusanywa iliwasilishwa kwa maelezo na kwa kutoa mifano ya maudhui, usawiri wa wahusika na mtindo kwenye tamthilia zilizoteuliwa. Mtafiti aliteua sampuli kimakusudi ili kufanikisha malengo ya utafiti. Utafiti ulikuwa wa maktabani ambapo mtafiti alisoma tamthilia husika, tasnifu, majarida na vitabu ambavyo vinahusiana na mada.