Maendeleo ya Tawasifu ya Kiswahili tangu Karne ya 19 hadi 21

Loading...
Thumbnail Image
Date
2023
Authors
Wabomba, Eric W.
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
Kenyatta University
Abstract
Utafiti huu umechanganua tawasifu tatu zilizoandikwa katika karne tatu tofauti ambazo ni: Tawasifu ya Tippu Tip iliyoandikwa karne ya 19 na kuhaririwa na Whiteley (1958), ya Shaaban Robert (1969) ya Maisha yangu na Baada ya miaka Hamsini, ya karne ya 20, na tawasifu ya Ken Walibora (2014) ya Nasikia sauti ya Mama, ambayo iliandikwa katika karne ya 21. Utafiti huu ulikuwa na malengo matatu ambayo ni: Kuchanganua vipengele vya uhalisia na ubunifu katika tawasifu ya Tippu Tip iliyohaririwa na Whiteley (1958); Kuchanganua vipengele vya uhalisia na ubunifu katika tawasifu ya Shaaban Robert (1969); Kuchanganua vipengele vya uhalisia na ubunifu katika tawasifu ya Ken Walibora (2014). Vipengele hivi vilichanganuliwa kwa kuangazia maudhui na mtindo wa uandishi uliotumika katika tawasifu hizi. Utafiti huu uliongozwa na nadharia mbili ambazo ni: Nadharia ya Uhalisia na nadharia ya Mtindo. Nadharia ya Uhalisia iliasisiwa na Hegel (1975 – 1979), Zola (1969) na Flaubert (1972), miongoni mwa wengine. Kwa mujibu wa nadharia ya Uhalisia, maisha ya jamii yanafaa kuwasilishwa kwa uaminifu na usahihi mkubwa. Mambo yanayoonekana katika jamii ndiyo hutiliwa mkazo. Nadharia ya Mtindo iliasisiwa na Buffon (1930) na kuendelezwa na waasisi wengine wakiwemo Wellek na Warren (1949), Coombes (1963), na Leech (1981). Nadharia hii huchunguza lugha ili kubainisha ubunifu uliomo kwenye lugha hiyo. Nadharia ya Uhalisia ilichaguliwa kuongoza utafiti huu kwa sababu, mwandishi yeyote wa tawasifu anatazamiwa kuelezea ukweli halisi kuhusu maisha yake. Kwa upande mwingine, nadharia ya Kimtindo ilichaguliwa kwa vile ambavyo tunatarajia mtunzi wa kinathari aelezee kiubunifu maisha yake akizingatia mbinu zinazoakisi ukweli, uzushi, chuku na kadhalika. Nadharia ya Uhalisia kwa upande mmoja, ilisaidia katika kuangalia viwango vya uyakinifu katika tawasifu hizi. Kwa upande mwingine, nadharia ya mtindo ilichangia katika kubainisha mtindo na ubunifu uliomo katika tawasifu hizi tatu. Mbinu za utafiti zilizotumiwa katika utafiti huu ni kusoma kwa kina, kueleza na kuchanganua vipengele vya mada. Data zilizotokana na utafiti huu zinabainisha viwango vya uhalisia na ubunifu na hivyo kuchangia pakubwa katika ujuzi wa tawasifu kama kipera cha riwaya. Watafiti wengine wanaopania kuzama katika uwanja wa tawasifu na uandishi wa kinathari kwa ujumla watafaidika kwa data za utafiti huu. Matokeo ya utafiti huu yatakuwa muhimu katika tafiti nyingine, haswa zile zitakazonuia kushughulikia uhalisia na ubunifu, sio tu katika tawasifu ya Kiswahili, bali katika tagaa la riwaya kwa ujumla.
Description
Tasnifu hii Imetolewa kwa Madhumuni ya Kutosheleza Baadhi ya Mahitaji ya Shahada ya Uzamili Katika Chuo Kikuu cha Kenyatta, June, 2023
Keywords
Maendeleo ya Tawasifu, Kiswahili, Kiswahili tangu Karne ya 19 hadi 21
Citation