Tathmini ya Maigizo ya Wahusika Walemavu Katika Kipindi cha Sultana Kwenye Runinga ya Citizen Nchini Kenya

Loading...
Thumbnail Image
Date
2025-09
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
Kenyatta University
Abstract
Kipindi cha Sultana kilipeperushwa kwenye runinga ya Citizen nchini Kenya kuanzia Machi, 2022 hadi Julai, 2023. Kipindi hicho kilihusisha wahusika mbalimbali wakiwemo walemavu. Tafiti za awali zimechunguza usawiri wa wahusika walemavu katika njia hasi. Utafiti huu ulilenga kuziba pengo hilo kwa kuchunguza usawiri wa wahusika walemavu kwenye vipindi vya televisheni kwa njia chanya. Hivyo basi, utafiti huu ulilenga kuchunguza maigizo ya wahusika walemavu kwenye kipindi hicho. Suala la utafiti lilikuwa kutathmini maigizo ya wahusika walemavu katika kipindi cha Sultana katika runinga ya Citizen nchini Kenya. Malengo ya utafiti huu yalikuwa; kujadili maudhui yanayowasilishwa na wahusika walemavu katika kipindi cha Sultana kwenye runinga ya Citizen, pili, kubainisha sifa za wahusika walemavu katika kipindi cha Sultana kwenye runinga ya Citizen na kufafanua mbinu za maigizo zinazotumika na wahusika walemavu katika kipindi cha Sultana kwenye runinga ya Citizen. Utafiti huu uliongozwa na nadharia ya Maigizo (Turner, 1969) inayosisitiza umuhimu wa kudhihirisha mitagusano ya wanajamii kwenye maisha yao halisi kupitia matendo yao kwenye jukwaa. Aidha, nadharia hii inaonyesha manufaa ya hadhira katika kuchunguza vitendo vya waigizaji kwenye jukwaa. Utafiti huu ulifanywa maktabani na nyanjani. Maktabani mtafiti alidurusu vitabu, majarida, tasnifu na miswada mbalimbali kuhusu uigizaji, mbinu za utafiti na nadharia ya Maigizo. Utafiti wa nyanjani ulihusu ukusanyaji wa data kwa kuhusisha mahojiano na kurekodi. Vifaa vya utafiti vilivyotumiwa ni simu ya rununu, tarakilishi na mwongozo wa mahojiano. Jumuiya ya utafiti ilikua waigizaji walemavu wa viungo na wa tabia wa kipindi cha Sultana cha runinga ya Citizen. Sampuli ya utafiti iliteuliwa kimaksudi ili mtafiti aweze kupata data ya malengo ya utafiti. Data ilikusanywa kwa kutazama, kusikiliza na kunukuu majibu ya maswali kutoka kipindi kiteule. Data ilichanganuliwa kwa njia ya maelezo kwa kuzingatia nadharia ya Maigizo, maswali na malengo ya utafiti. Matokeo ya utafiti yaliwasilishwa kimaelezo. Utafiti ulibaini kuwa wahusika walemavu wa viungo na wa tabia wanawasilisha maudhui mbalimbali. Wahusika walemavu wanawasilisha maudhui ya bidii, mapenzi, ujasiri na unyanyapaa ilhali wale wa tabia wanawasilisha maudhui ya ukatili, mauaji, tamaa na utabaka. Utafiti pia umeonyesha kuwa wahusika walemavu wana sifa mbalimbali wanazotumia kuwasilisha maudhui. Wahusika walemavu wa viungo wanadhihirisha kuwa na ukakamavu, hasira, ubinafsi, upweke, uvumilivu na hekima ilhali wale wa tabia wanadhihirisha kuwa na taasubi ya kiume, ukatili, udanganyifu, tamaa, ukaidi na uchochezi. Aidha, mbinu mbalimbali zilitumiwa na wahusika walemavu. Mbinu hizi ni pamoja na kufananisha, ishara za mwili, mazungumzo na hisia na mielekeo ya wahusika. Utafiti huu utasaidia kuongeza data muhimu katika taaluma ya fasihi. Pia, utawafaa watafiti watakaotumia nadharia ya Maigizo kwa kurejelea mihimili yake ambayo mtafiti amejadili kwa kina.
Description
Tasnifu Hii Imewasilishwa Katika Shule ya Sheria, Sanaa na Sayansi za Kijamii Ili Kutosheleza Baadhi ya Mahitaji ya Shahada ya Uzamili Katika Chuo Kikuu cha Kenyatta. Septemba, 2025 Msimamizi Richard Makhanu Wafula
Keywords
Citation