Mikakati na mbinu za usimilishwaji katika fasihi ya watoto

Loading...
Thumbnail Image
Date
2012-01-04
Authors
Muthubi, Fidelis M.
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
Abstract
Utafiti huu umeshughulikia usimilishwaji wa kazi za watoto katika fasihi ya watoto ya Kiswahili. Lengo la utafiti huu ni kuainisha na kufafanua mikakati na mbinu zinazotumika katika kusimilisha kazi za watoto. Kadhalika utafiti huu umetumia mbinu hizi kuvihakiki vitabu vifuatavyo: Alfu lela ulela, Mashimo ya Mfalme Sulemani na Mkasa wa Shujaa Liyongo. Nadharia iliyoongoza utafiti huu ni nadharia ya Elimumitindo. Nadharia hii huzingatia lugha na matumizi yake katika kazi za fasihi. Aidha nadharia hii huchunguza mtindo wa mwandishi kama unavyojitokeza katika kazi zake. Tasnifu hii imegawanywa katika sura saba. Sura ya kwanza imeshughulikia mada ya utafiti, madhumuni ya utafiti pamoja na sababu za kuchagua mada hii. Kadhalika, udurusu wa maandishi yanayohusu mada ya utafiti pamoja na msingi wa nadharia iliyoongoza utafiti huu ni baadhi ya mambo ambayo yameshughulikiwa. Sura ya pili inahusu mikakati na mbinu zinazozingatiwa wakati mwandishi anaisimilisha kazi yake. Mbinu hizi zimeainishwa na kufafanuliwa. Maelezo haya ni muhimu kwani ndiyo yametumiwa kama msingi wa kuchanganua kazi zilizoteuliwa. Sura ya tatu imekihakiki kitabu cha Alfu Lela Ulela. Uhakiki huu unabainisha jinsi usimilishwaji wa ngano (za fasihi simulizi) ambazo zilitambwa na watu wazima kwa hadhira ya watu wazima zinasimilishwa kuwa kazi zinazoilenga hadhira ya watoto. Sura ya nne imeihakiki riwaya ya Mashimo ya Mfalme Sulemani Uhakiki huu ni muhimu kwani unabainisha jinsi kitabu kinachoilenga hadhira ya watu wazima kinasimilishwa na kuilenga hadhira ya watoto. Sura ya tano imeihakiki riwaya ya Mkasa wa Shujaa Liyongo. Uhakiki huu unatupa picha kamili ya jinsi tenzi zinasimilishwa kuwa hadithi za kusomwa na watoto. Sura ya sita inahusu ulinganishi na ulinganuzi wa vitabu vyote vitatu vilivyoshughulikiwa katika utafiti huu ili kuwa na picha kamili ya mwelekeo wa usimilishwaji wa kazi za watoto. Sura ya saba ni hitimisho la tasnifu hii. Mambo ambayo yamezingatiwa ni pamoja na muhtasari, matokeo, matatizo na mapendekezo ya mtafiti.
Description
The PL 8704.M8M5
Keywords
Children literature--History and Criticism//Children literature--Swahili--Kenya//Children literature--Swahili--Kenya--Study and teaching
Citation