Ufungamano wa Itikadi na Propaganda Katika Tamthilia za Kithaka wa Mberia: Kifo Kisimani (2001) na Maua Kwenye Jua La Asubuhi (2004)

Loading...
Thumbnail Image
Date
2023
Authors
Minyade, Sheril Mugaduka
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
kenyatta university
Abstract
Utafiti huu umeonyesha ufungamano wa itikadi na propaganda katika tamthilia za Kithaka Wa Mberia: Kifo Kisimani (2001) na Maua kwenye Jua la Asubuhi (2004). Baadhi ya sababu ambazo zimechochea kufanywa kwa utafiti huu ni kuwa; suala la itikadi ni la muhimu sana kwa vile ndilo ambalo huongoza matendo ya binadamu. Pia, propaganda ina uhusiano wa karibu sana na kazi za kifasihi ambazo huwa ni chombo cha kiitikadi. Kwa hivyo, malengo ya utafiti yalikuwa kubainisha aina za itikadi katika tamthilia teule, kuonyesha aina za propaganda katika tamthilia teule na kuonyesha uhusiano kati ya itikadi na propaganda. Kwa mujibu wa Marx na Engels (1977), itikadi ni fikra zote za maoni ya wanadamu kuhusu wanayoyasema na wanayoyafikiria kuhusu dini, sheria, siasa, maadili na falsafa. Propaganda hushawishi fikra za mtu kutenda jambo kwa namna fulani. Ni ushawishi unaoratibiwa kwa malengo fiche, (Ellul, 1965). Tamthilia za Kifo Kisimani na Maua kwenye Jua la Asubuhi ziliteuliwa kimaksudi kwa sababu zina data ambayo imetumika katika kutimiza malengo ya utafiti. Utafiti huu umeongozwa na nadharia ya Uchanganuzi Tahakiki Usemi (UTU) iliyoasisiwa na Fairclough (1989). Ni nadharia ambayo hueleza uhusiano uliopo kati ya matukio ya kiusemi, kisiasa, kijamii na kiutamaduni na jinsi yanavyoathiriwa na itikadi.Nadharia teule inaangazia jinsi usemi huo huathiri matukio katika jamii. Utafiti huu ni wa kimaelezo kwa sababu uchanganuzi wa data umetekelezwa na kuwasilishwa katika maelezo ya kina. Kutokana na maelezo ya kina, itikadi ya dini, ukombozi, utawala, utamaduni, umwinyi na ubepari imebainishwa kutoka katika tamthilia teule. Data ilikusanywa kutokana na muktadha wa mazungumzo ya wahusika, usemi na matumizi yao ya lugha. Mtafiti ameonyesha aina za propaganda kama vile propaganda ya kisiasa na kijamii, wazi, siri na propaganda ya kati. Pia, utafiti umethibitisha kuwa itikadi na propaganda ni dhana mbili tofauti lakini zina uhusiano wa karibu. Diskozi zote zinaongozwa na itikadi ambapo maudhui, usemi, matumizi ya lugha na muktadha wa mazungumzo huashiria itikadi ya mhusika. Propaganda na itikadi ni masuala muhimu katika kazi za kifasihi. Hata hivyo, imebainika kuwa ili propaganda iweze kufaulu, inajiegemeza katika itikadi fulani. Pia, hakuna itikadi ambayo inaweza kufaulu bila kuwashawishi watu. Ushawishi huu ndio propaganda, na hivyo kufanya dhana hizi kuwa na uhusiano wa karibu sana. Tafiti zaidi zinaweza kufanywa katika kitengo cha itikadi ili kuchunguza wahusika wanaharakati katika tamthilia hizi. Uanaharakati unaendana moja kwa moja na itikadi ambayo huhalalisha seti za matendo zinazojitokeza katika vitendo. Utafiti huu unawawezesha wasomi na wahakiki wa kazi za kifasihi kutumia dhana ya itikadi na propaganda kama dhana mbili tofauti ambazo zina ufungamano.
Description
Tasnifu hii Imewasilishwa ili Kutosheleza Baadhi ya Mahitaji ya Shahada ya Uzamili Katika Chuo Kikuu cha Kenyatta
Keywords
Itikadi na Propaganda, Kithaka wa Mberia, Kifo Kisimani, Maua Kwenye Jua La Asubuhi
Citation